BAN KI-MOON AELEZA KUSIKITISHWA NA JINAI ZINAZOFANYA NA ISRAEL

Umoja wa Mataifa umesisitiza kuwa katika vita vya siku 50 vilivyoanzishwa na utawala wa Kizayuni wa Israel dhidi ya Ukanda wa Gaza shule saba za umoja huo zilishambuliwa, na Wapalestina 44 waliuliwa kwenye mashambulio hayo.

Katika barua aliyoandika na kuiambatanisha na ripoti ya matokeo ya uchunguzi kuhusu vita vya Gaza ambayo ilitolewa siku ya Jumatatu, Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Ki-moon amesema, na hapa ninamnukuu:"Ninasikitishwa na ukweli huu, kwamba Wapalestina wasiopungua 44 waliuliwa na wengine 227 walijeruhiwa katika mashambulio iliyofanya Israel kwenye vituo na majengo ya elimu ya Umoja wa Mataifa yaliyotumiwa na watu hao kama vituo vya kupatia hifadhi ya dharura".
Matukio yanayojiri kimataifa yanaonyesha kuwa jinai za Israel dhidi ya wananchi wa Palestina zingali zinaendelea kufuatiliwa kimataifa. Kuendelea kutolewa radiamali dhidi ya jinai za utawala wa Kizayuni ni ithbati na ushahidi tosha wa kuonyesha kuwa utawala huo ghasibu umeshindwa kuficha na kufifilisha jinai zake hizo na kwamba jinai za kinyama na za kutisha zinazofanywa na Israel haziwezi kufutika ndani ya fikra za walimwengu.
Wito ambao umekuwa ukitolewa kutokea pembe mbalimbali za dunia wa kutaka kuchunguzwa jinai za Israel na kuwachukulia hatua watenda jinai wa Kizayuni ni ishara ya kushtadi harakati za kimataifa za kutaka zichukuliwe hatua za kisheria dhidi ya utawala huo usio na chembe ya utu na unaonuka kimataifa kutokana na jinai zake.
Itakumbukwa kuwa Wapalestina wasiopungua 2,200 walipoteza maisha na maelfu ya wengine walijeruhiwa wakati wa vita vya siku 50 vya mwaka 2014 vilivyoanzishwa na utawala wa Kizayuni wa Israel dhidi ya Ukanda wa Gaza. Aidha nyumba elfu 89 za Wapalestina ziliharibiwa, elfu 15 miongoni mwa hizo zikiwa zimebomolewa kabisa au kuharibiwa kwa kiwango cha kutoweza kukalika tena.
Mbali na maelfu hayo ya nyumba za raia, zaidi ya shule 140 na majengo ya viwanda 350 pia yalibomolewa na kuifanya hali ya eneo la Gaza lililowekewa mzingiro na utawala haramu wa Israel iwe mbaya zaidi. Mwenendo wa Israel unadhihirisha jinsi utawala huo khabithi usivyojali wala kuchunga mipaka yoyote katika kutenda jinai zake.
Kitendo cha utawala huo ghasibu cha kupuuza maazimio ya Umoja wa Mataifa na kukiuka kila mara mikataba ya kimataifa kimeitafiri na kuichosha Jamii ya Kimataifa. Kuitishwa vikao mbalimbali vya kimataifa kuhusiana na jinai za utawala wa Kizayuni na kutolewa maazimio, taarifa na ripoti kadha wa kadha za Umoja wa Mataifa na taasisi zenye mfungamano na umoja huo dhidi ya Israel ni ushahidi kwamba walimwengu wanakabiliana na utawala afriti na uliokubuhu katika kutenda jinai.
Katika hali na mazingira kama hayo kutochukua hatua yoyote Umoja wa Mataifa dhidi ya Israel na kutosheka na kutoa ripoti tu kuhusiana na jinai za utawala huo haramu hakutokuwa na tija nyengine ghairi ya kushadidisha vitendo vyake haribifu unavyovifanya kieneo na kimataifa. Kutolewa ripoti ya uchunguzi kuhusu jinai za Israel katika vita vya siku 50 vya mwaka 2014 huko Gaza ni muendelezo wa ripoti ya kamati ya kutafuta ukweli iliyoongozwa na Jaji Richard Goldstone ambayo ilifanya uchunguzi kuhusu vita vya siku 22 vilivyoanzishwa na utawala wa Kizayuni pia dhidi ya Wapalestina wa Ukanda wa Gaza mnamo mwaka 2009.
Ripoti hiyo iliyotokana na ushahidi wa nyaraka elfu 20, picha na mazungumzo ya ana kwa ana na mashaidi zaidi ya 200 ilithibitisha kwa uwazi kabisa kwamba utawala wa Kizayuni ulitenda jinai za vita katika mashambulio yake ya siku 22 dhidi ya Gaza.
Lakini pamoja na kamati ya Jaji Goldstone kutoa ushahidi huo, ukwamishaji uliofanywa na Marekani na baadhi ya madola ya Magharibi pamoja na upuuzaji wa Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa katika ufuatiliaji, ripoti hiyo ya kamati ya kutafuta ukweli haikusaidia kuchukuliwa hatua yoyote ya kivitendo dhidi ya Israel; na kwa kweli ni mwenendo huo ndio unaozidisha kiburi na jeuri ya utawala haramu wa Kizayuni ya kuendelea kufanya jinai utakavyo.

Katika hali kama hiyo kutosheka viongozi wa Umoja wa Mataifa akiwemo Katibu Mkuu wake na kutoa matamshi matupu ya kulaani jinai za Israel hakutokuwa na matokeo mengine zaidi ya kuufanya utawala huo uendeleze jinai zake zinazozidi kuungulisha na kusononesha nyoyo za fikra za waliowengi duniani
Share on Google Plus

About Rafiki Fm Ludewa

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments: