WAZIRI MAGUFULI AZUIA BOMOABOMOA MKOANI KILIMANJARO


Waziri wa Ujenzi Dkt. John Magufuli ametangaza kutobomoa nyumba zilizopo kando kando ya  barabara ya Mwanga-Kikweni/Vuchama-hadi Lomwe km 40.6 na kusema kuwa barabara hiyo itajengwa kwa kiwango cha lami kwa kutumia upana wake uliopo sasa hivi.

Dkt. Magufuli alitoa kauli hiyo ya faraja kwa wakazi wa Kikweni Wilayani Mwanga Mkoani Kilimanjaro kabla ya kuweka jiwe la msingi katika barabara ya Mwanga-Kikweni/Vuchama-Usangi hadi Lomwe(km 40) itakayojengwa kwa kiwango cha lami hivi karibuni.

Waziri wa Ujenzi amechukua uamuzi huo kutokana na maeneo mengi ya milimani ambapo barabara hiyo inapita kuwa na mashamba ya watu tofauti na sehemu nyingine. “Nikiwa kama Waziri wa ujenzi katika maeneo haya ya milima sitatumia sheria ya mita 30 kila upande katika ujenzi wa barabara hii ili nyumba na mashamba ya wakazi wa huku yasiathirike”.

Dkt. Magufuli aliongeza kuwa ujenzi wa Barabara una sheria zake ndio maana ameamua kutumia sheria ya barabara  namba 13 ya mwaka 2007 kifungu cha 13 na 20 kinachompa mamlaka kupunguza upana wa barabara.

Aidha, Waziri Magufuli aliwatoa hofu wakazi wote waliowekewa alama ya X katika nyumba zao na kuwataka kuendelea na shughuli zao kama kawaida kwasababu nyumba hizo hazitabomolewa.

Katika hatua nyingine Dkt. Magufuli aliwataka watu wote waliojenga vibanda karibu na barabara ya zamani waanze kuondoka mapema kabla ya ujenzi wa barabara hiyo kuanza hivi karibuni.

“Nawaomba wote mlioweka vibanda karibu na barabara mtoe kwa hiari yenu ili tutengeneze barabara hii bila vikwazo na kwa haraka tofauti na awali ambapo tulikuwa tunatangaza zabuni kwa kilomita chache” alisisitiza Waziri Magufuli.

Kwa upande wa Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro Leonidas Gama amemshukuru Waziri Magufuli kwa hatua yake hiyo na kusema kuwa kufunguka kwa barabara hiyo ni mkombozi mkubwa kwa wilaya ya Mwanga na Mkoa wa Kilimanjaro kwa ujumla.

“Wilaya yetu hii inapakana na nchi jirani hivyo hata kiusalama ni vizuri barabara hii ikajengwa kwa lami ili irahisishe mawasiliano kwa haraka zaidi katika Wilaya yetu hii” alisema Mkuu wa Mkoa.

Naye Mbunge wa Mwanga ambaye pia ni Waziri wa Maji Profesa Jumanne Maghembe ameishukuru Serikali na kusema kuwa kukamilika kwa barabara hiyo kutawaondolea kero kubwa ya usafiri wananchi wa Usangi na mwanga na kuwasaidia kufanya biashara kwa urahisi zaidi tofauti na awali.

“Kukamilika kwa barabara hii kutasaidia kuinua uchumi mkubwa uliopo huku Usangi tofauti na hali iliyopo sasa” Alisema Profesa Maghembe
Share on Google Plus

About Rafiki Fm Ludewa

This is a short description in the author block about the author. You edit it by entering text in the "Biographical Info" field in the user admin panel.
    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments: