
Alikuwa yuko Bar moja maarufu iliyoko maeneo ya Kinondoni hapa jijini Dar na hawara yake ambaye ndio nyumba yake ndogo pamoja na marafiki zake kadhaa wakikata maji (Pombe), Bwana Tesha (sio jina lake halisi) alikuwa na furaha siku hiyo kwani alikuwa amefanikiwa kupata tenda moja ya bajeti kubwa ambayo ilimhakikishia kupata faida ya kutosha.
Bwana Tesha anamiliki kampuni yake ya Ujenzi hapa jijini na alikuwa bado ni kijana mdogo, lakini kwa muda mfupi tangu amalize masomo yake ya Chuo Kikuu pale Mlimani alimudu kujiajiri katika sekta ya ujenzi na kupata mafanikio makubwa katika sekta hiyo.
Akiwa bado anakata maji na marafiki zake pamoja na hawara yake alipigiwa simu na mkewe. Kwa kuwa kulikuwa na kelele za walevi katika Bar hiyo aliamua kwenda kupokelea simu ile ndani ya gari lake. Simu ile haikuwa na taarifa nzuri, alijulishwa na mkewe kuwa mama mkwe wake yaani mama wa mkewe amefariki ghafla kwa presha huko Moshi mkoani Kilimanjaro.
Alirudi kwenye meza aliyokuwa amekaa ma wenzie na kuwajulisha juu ya taarifa ile, wenzie walimpa pole na kumshauri arudi nyumbani ili kumfariji mkewe. Hata hivyo alilazimika kwanza kumpeleka hawara yake nyumbani kwake maeneo ya Mwenge ndipo aende nyumban kwake maeneo ya Mbezi ya Kimara.
Wakati huo hawara yake alikuwa amelewa chakari na alikuwa hajitambui, hivyo ilimlazimu kumbeba na kumuingiza ndani ya gari yake aina ya Toyota RAV 4. Aliondoka hadi kwa hawara, aliteremka na kufungua mlango wa nyumba kisha akambeba hawara yake ambaye alikuwa hajitambui hadi ndani na kumlaza kitandani. Kwa kuwa alikuwa na funguo za akiba, alifunga mlango na kuondoka zake kuwahi nyumbani kwake.
Alifika nyumbani kwake majira ya saa nne usiku, na kukuta baadhi ya ndugu zake na ndugu wa mkewe. Baada ya mashauriano, walikubaliana yeye na mkewe waondoke kesho alfajiri, kwa kuwa yeye hahitaji kuomba ruhusa kazini.
Baadhi ya ndugu zake na ndugu wa mkewe alipanga kuondoka baadae na mabasi baada ya kuomba ruhusa kazini kwao. Walifungasha haraka haraka usiku huo huo kisha wakalala. Ilipofika alifajiri ya saa kumi za usiku waliondoka kuelekea Moshi. Ndani ya gari walikuwa wanne, mwanae wa kwanza wa kiume aliyekuwa na umri wa miaka 12 alikaa kiti cha mbele, mkewe pamoja na mwanae mwingine wa pili wa kike aliyekuwa na miaka 7 walikaa kiti cha nyuma. Kwa kuwa bado walikuwa na usingizi, wote walilala, na kutokana na ufinyu wa nafasi mama aliweka miguu yake katikati ya viti vya mbele na kujiegemeza kwa nyuma akimuacha mwanae wa kike amlalie mapajani mwake.
Mzee Tesha aliendesha gari kwa tahadhari sana ili kuepuka ajali. Wakati kunapambazuka alikuwa amekaribia maeneo ya mto Wami, na alijisikia kubanwa haja ndogo. Alilazimika kusimama na kuteremka ili kuchimba dawa. Alimaliza kuchimba dawa na kurejea ndani ya gari, lakini kabla ya kuondoa gari akashangaa kuona kiatu kinachofanana na kile alichovaa hawara yake usiku wa jana kikiwa chini ya kiti cha mbele cha abiria. Bwana Tesha akashtuka, akajua kile ni kiatu cha hawara yake ambaye atakuwa amekiacha mle katika gari kwa kuwa alikuwa amelewa chakari. Akageuka na kumwangalia mkewe aliyekuwa amelala kiti cha nyuma.
Aliwakagua wote ili kutaka kujua kama wamelala, na alipohakikisha kuwa wote wamelala, alikichukua kile kiatu na kukitupilia mbali, kisha akaondoa gari, akiwa amefarijika kuwa kiatu kile hakijaonwa na mkewe ambaye wanaaminiana sana tangu waoane miaka kumi iliyopita.
Aliendesha gari kwa mwendo wa wastani na ilipofika saa nne asubuhi walikuwa wako Segera, walisimama pale ili kupata staftahi. Baada ya kupaki gari aliteremka na wanae wawili na kutangulia mghahawani na kumwacha mkewe nyuma akijiweka sawa kabla ya kuteremka ndani ya gari.
Akiwa ndani ya mghahawa mkewe alimpigia simu na kumtaka aende kwenye gari kuna dharura, alitoka mghahawani na kumfuata mkewe kule kwenye gari, ili kujua kulikoni. Alipofika, alishtuka kumkuta mkewe kashikilia kiatu kimoja kinachofanana na kile alichokuwa amevaa hawara yake usiku wa jana walipokuwa kule Bar, akajua siri imefichuka, lakini akawahi kuficha mshtuko wake, na kumuuliza mkewe, “Vipi kuna nini mke wangu?”
Mkewe akamwambia kuwa ameshangaa haoni kiatu chake kimoja. Bwana Tesha akajua kiatu kisichoonekana ni kile alichokitupa kule mto Wami. Lakini alikuwa mwerevu….
“Mke wangu ana uhakika ulivaa viatu vyote viwili?” Alimuuliza mkewe akiwa na mshangao.
“Mume wangu pamoja na kuwa nimefiwa na nina uchungu sana lakini sijapoteza fahamu zangu kiasi cha kujisahau na kuvaa kiatu kimoja.” Mkewe alimjibu kwa upole.
Bwana Tesha alijifaragua akijifanya anakitafuta kiatu cha mkewe kwa bidii hasa, baada ya kupekua sana alikuja na ushauri mwingine, ambapo alimshauri mkewe wanunue kandambili avae kwa muda kwa madai kuwa wakifika Moshi watakitafuta kwa umakini.
Mkewe alikubali, lakini bado alikuwa na mashaka kidogo juu ya tukio lile. Walinunua kandambili na baada ya kupata kiamsha kinywa waliondoka. Walipofika Korogwe, Bwana Tesha alisimama na kwenda dukani ambapo alimnunulia mkewe Viatu vingine kisha wakaondoka kuwahi Mazishi.
Baada ya kufika Moshi habari ya upotevu wa kiatu kimoja ilisimuliwa na cha kushangaza tukio lile likahusishwa na mambo ya kishirikiana sambamba na msiba ule. Na hiyo ndio ikawa ndio salama ya Bwana Tesha kuepukana na fedheha ile ya kutupa kiatu cha mkewe baada ya kukifananisha na kiatu cha hawara yake.
Ludewa yetu na maendeleo yetu posted by barnabas njenjema, kutoka Ludewa
0 comments:
Post a Comment